Watu sita wamejeruhuiwa kwa mapanga sehemu mbalimbali za miili yao
Wilayani Tarime mkoani Mara akiwemo mwandishi wa habari wa Sahara
Media, Geoge Nteminyanda (49) usiku wa kuamkia leo.
Wakizungumza na mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi katika wodi
namba tatu na namba nane walikolazwa, majeruhi hao wamesema kuwa
walishambuliwa na wafuasi wa vyama vya Chadema na CCM ambao walikuwa
katika makundi makundi kati ya saa mbili na saa nne usiku.
Nteminyanda ambaye ni mkazi wa Kisesa Mwanza amesema kuwa aliitwa na
mgombea ubunge wa CCM, Michael Kembaki na kufikia katika hoteli ya CMG
ambapo kulikuwa na kikao cha chama hicho lakini alianza kuhojiwa na
baadhi ya wanachama wa chama hicho. Lakini licha ya kutoa vitambulisho
vya kazi wafuasi hao walianza kumshambulia kwa kumpiga mapanga mwilini
na kuanguka chini. Hata hivyo watu hao waliendelea kumkanyaga hadi
akapoteza fahamu.
Wasamaria wema walimchukua na kumpeleka hospitalini ambapo alipewa kitanda namba tatu cha wodi namba tatu.
“Waliokuwa wakinishambulia walikuwa vijana wengi kutokana na kunikabiri
vibaya sikuwatambua kwa haraka lakini wakiwekwa kwenye mstari wa
utambuzi nitawatambua” amesema Nteminyanda.
Wengine waliojeruhiwa ni Waiboga warioba (37) aliyekatwa kichwa na sikio
la kulia,Busiro Rhobi (28) mkazi wa Nyamongo aliyekuwa na gari lake
binafsi, Daniel Mathew (18) mkazi wa Goribe Wilayani Rorya anayedaiwa
kupigwa risasi kichwani upande wa kulia na mgombea udiwani wa kata ya
Ikoma Laurence Andriano (CCM).
Wengine ni Wambura Marai (38) aliyeopolewa kutoka kwenye gari lake baada
ya kutokea ubishani kati yake na wafuasi wa CHADEMA kuwa mshindi urais
atakuwa John Pombe Magufuli.
Rose Hosea muuguzi mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya Tarime amesema kuwa
wakati wanapokelewa hali yao ilikuwa mbaya zaidi lakini kutokana na
juhudi za timu ya wauguzi wa zamu walitoa huduma za haraka ikiwa ni
pamoja na kuwashona majeraha yao huku wakiwapa dawa za maumivu.
“Hali yao inaendelea vizuri kwa sasa tofauti na ilivyokuwa jana” amesema Hosea.
Tagged with: MATUKIO
Hakuna maoni :