SIASA

SIASA

MAONI

MAONI

BURUDANI

MICHEZO

/ / ONDOKA YA SAMATTA NI SHEREHE, AJABU HAKUNA ANAYEJIANDAA KUSAFIRI NAYE





UMESIKIA mshambuliaji nyota wa TP Mazembe, Mbwana Samatta anaondoka zake kwenda zake Nigeria kwa ajili ya shughuli ya utoaji wa tuzo za wachezaji bora barani Afrika?

Tuzo hizo zinafanyika Januari 7, mwakani. Samatta ataondoka Januari 5 na hali halisi inaonyesha anaweza kuibuka na ushindi kwa kuwa ana nafasi.

Nafasi yake inatokana na kazi kubwa aliyoifanya akiwa na TP Mazembe na kuiwezesha kubeba ubingwa wa Afrika. Alifunga mabao katika mechi zote za fainali, pia ameibuka kuwa mfungaji bora na kupata nafasi ya kucheza Kombe la Dunia la Klabu nchini Japan.

Hiyo ni safari ya kwanza ya Samatta, safari ya pili nayo inatarajia kuwa mapema mwakani, anatarajiwa kwenda nchini Ubelgiji kujiunga na Klabu ya Genk ya nchini humo.

Samatta ameishamalizana na Genk kwa maana ya makubaliano, anachosubiri ni TP Mazembe kumalizana Genk ili yeye amalizane pia na Wabelgiji hao walioonyesha kweli wako makini walipoamua kuja hadi jijini Dar es Salaam na kuzungumza na baba yake na familia yake kwa jumla, lakini wakamfuata hadi Japan.

Samatta ana safari mbili, kwanza tumuombee kwa Mwenyezi Mungu afanikiwe kwa kuwa tayari ameonyesha ni mtu mwenye juhudi, anajitambua na amegeuka kuwa alama ya taifa letu unapozungumzia soka huku akiwa ni mchezaji aliyeibuka juzijuzi tu.

Wakati Samatta anafunga safari hizo, nani amejipanga kuondoka naye? Nani amejipanga angalau baadaye kusafiri safari kama hizo hapo baadaye? Au ndiyo watu wanafurahia tu na kugeuza kinachofanyika ni kama filamu ambayo baada ya picha yanafuatia majina ya waigizaji na wahusika wengine?

Safari ya Samatta haikuwa ya kuotea tu, alianza kwa hatua, alipambana, alikuwa na malengo au ndoto na alitaka kuzitimiza. Hadi sasa bado hajatimiza lakini akiwa njiani anapita katika barabara ya asali ambayo inamfanye awe tofauti na wengi.

Samatta amekuwa tofauti na wale waliokuwa mastaa, nyota wa miaka nenda rudi na wengine sasa wamekuwa kama wendawazimu, siku zinavyokwenda wanadidimia na vipaji vyao kwenda timu za chini au madaraja ya chini, “wanakufa na vipaji vyao.”

Samatta si malaika, si anayejua mpira kuliko Watanzania wote, lakini ukweli nidhamu, kujituma na nia ya kufikia anachokitaka, vimembeba na kubadilisha maisha yake. Tukubali huyu Samatta si yule wa Mbagala Market, African Lyon wala Simba. Je, unakumbuka ni miaka mingapi imepita? Tangu wakati huo nyota wangapi unawajua hadi leo wamesahaulika kabisa?

Ndiyo maana nikauliza hivi, nani anataka kuondoka na Samatta? Nikiwa ninamaanisha hivi mwenye hamu ya mafanikio anayopata na mwenye kutaka kuyafikia kwa kupambana kwa kuweka nia, kujituma na kujitambua.

Nani anataka kubadilika? Kutoka wale mastaa wetu wa enzi zile au wa hivi karibuni ambao maisha yao hadi leo hayako vizuri kwa kuwa wamekuwa watu wa kubahatisha tu wakati walikuwa na vipaji lakini waliona Yanga na Simba ndiyo mwisho wa reli!

Samatta amefika alipo lakini haikuwa safari rahisi au laini. Hakika amepambana na anayetaka kumfuata lakini akubali kupambana pia kufikia alipo na si kulala na kutamani halafu akiamka tayari awe Samatta, itakuwa ni kujidanganya.

Mafanikio ya bila jasho ni yale ya haraka, yasiyojengwa na huporomoka haraka na hayana muda mrefu. Wakati Samatta anaondoka, najua wengi sana mnatamani au kumtamani angalau kufikia TP Mazembe na mafanikio aliyopata.

Basi anzeni sasa, si kusubiri umri ukishawatupa mkono, ndiyo muanze kukumbuka. Lazima mkubali kuumia, nidhamu pia iwabebe ili kufikia hapo ili siku nyingine Mwenyezi Mungu akijaalia, nanyi muondoke kama yeye, tuwasindike kwa pongezi na kiu ya kufikia mlichokifikia.

SOURCE: CHAMPIONI

«
Next

Chapisho Jipya

»
Previous

Taarifa za zamani

About Unknown

Asante kwa kutembelea SELASINI HABARI,NITAKUHABARISHA, KUKUELIMISHA NA KUKUBURUDISHA HIVYO USIKOSE KUTEMBELEA SELASINIHABARI.BLOGSPOT.COM.

Hakuna maoni :

Leave a Reply