SIASA

SIASA

MAONI

MAONI

BURUDANI

MICHEZO

/ / Kiama cha Mtandao wa Matajiri Wauza Madawa ya Kulevya 'Unga' Kimefika....Sasa ni Pekua Pekua na Kumata tu

Siku za wauza unga sasa zinahesabika baada ya Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya kuvunjwa rasmi na chombo kingine kitakachokuwa na mamlaka ya kuchunguza, kukamata, kupekua, kuteketeza na kuwapeleka mahakama kikitarajiwa kuundwa hivi karibuni.

Hatua hiyo imekuja baada ya Sheria ya Dawa za Kulevya ya mwaka 1995 kufikia kikomo Septemba 14 na kutungwa kwa sheria mpya ya kupambana na dawa za kulevya ya mwaka 2015 iliyoanza kutumika Septemba 15, mwaka huu.

Machi mwaka huu, aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Jenista Mhagama wakati akisoma muswada wa Sheria ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya (the drug control and enforcement act, 2014) bungeni Dodoma, alisema Serikali inakusudia kuanzisha chombo kinachojitegemea chenye mamlaka ya kiutendaji ya kuchunguza, kupekua na kukamata watuhumiwa tofauti na ilivyokuwa tume ambayo haikuwa na mamlaka ya kudhibiti na kupambana na tatizo hilo.

Katika mapambano hayo dhidi ya dawa za kulevya tofauti na sheria inayotumika sasa, chombo hicho kitajikita katika maeneo muhimu ikiwamo; kudhibiti mbegu za mimea ya dawa za kulevya, kuongeza viwango vya faini na nyongeza ya kifungo badala ya kuwa mbadala wa kifungo, na kutoa adhabu kutokana na uzito wa kosa.

Mapendekezo yaliyotolewa na kwa mujibu wa Muswada huo, watakaobainika kufanya biashara ya dawa za kulevya watozwe faini ya Sh1 bilioni moja au kifungo kisichopungua miaka 30 jela.

Pia, atakayekutwa analima, kusambaza mbegu, kusafirisha, kuzalisha au kuingiza mimea inayozalisha dawa za kulevya kama bangi, mirungi na cocaine atatozwa faini isiyopungua Sh 20milioni, kifungo kisichozidi miaka 30 au vyote pamoja.

Akiwa kwenye mikutano ya kampeni, Rais John Magufuli alitangaza mapambano dhidi ya dawa za kulevya na alipozindua Bunge Novemba 20, aliwaomba Watanzania wamuombee katika mapambano hayo aliyoyasema kuwa ni magumu.

Wakati akihutubia Bunge mjini Dodoma, Rais Magufuli alisema dawa za kulevya ni janga kwa taifa na kundi linaloathirika zaidi ni vijana wa kiume na kike.

Aliongeza kusema kuwa familia nyingi zimeathirika na nguvu kazi ya taifa imepotea kutokana na matumizi ya dawa hizo za kulevya.

“Tutaushughulikia mtandao huo hususan wafanyabiashara wakubwa wanaojihusisha na dawa za kulevya bila ajizi,” alisema.

Hata hivyo, hadi sasa uundwaji wa chombo kipya haujakamilika hadi Rais atakapomteua kamishna wa kukiongoza.

Msemaji wa tume hiyo, Florence Mlay, alisema tume ipo katika hatua za mabadiliko kuelekea kuwa chombo kamili kutokana na sheria mpya ya mwaka 2015.

“Hiki chombo kitakuwa na mabadiliko na kitakuwa na majukumu makubwa zaidi tofauti na ilivyokuwa tume,” alisema.

Katika miaka ya 90, Serikali ilianzisha vitengo vya kudhibiti dawa za kulevya katika baadhi ya idara na taasisi zake ili kuimarisha jitihada za udhibiti wa dawa za kulevya nchini.

Taasisi hizo ni Jeshi la Polisi, Idara ya Usalama wa Taifa na Idara ya Ushuru wa Forodha. Pamoja na jitihada hizo, tatizo la dawa za kulevya limeendelea kukua, mwaka 1995, Bunge lilitunga Sheria ya Kuzuia Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Namba 9 ya Mwaka 1995 (Sura 95).

Sheria hiyo ilianzisha Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya ambayo ilianza kazi mwaka 1997, chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na mwenyekiti wa Tume ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumzia sheria mpya ya dawa za kulevya, Mkuu wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya nchini, Alfred Nzowa alisema katika sheria mpya, dawa za kulevya hazihifadhiwa kama ilivyo sasa bali zitaharibiwa baada ya kupata hati ya uthibitisho kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.

“Tume haipo tena hii ni baada ya kuundwa kwa sheria mpya, lakini chombo kipya kitakachoundwa kitakuwa na meno zaidi ya tume na kitakuwa na vitengo hadi mikoani,” alisema.

Alisema sheria hiyo mpya ya dawa za kulevya haijaathiri kitengo cha kupambana na dawa za kulevya kwa kuwa kimeundwa na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP).

Kesi 105 za dawa za kulevya

Akizungumzia kesi za dawa za kulevya nchini, Kamanda Nzowa alisema mpaka sasa bado kesi 105 zipo katika hatua ya kusikilizwa na watuhumiwa wengine wamehukumiwa.

Nzowa alitoa mfano wa Anna Mboya kuwa alikamatwa Novemba 2, 2011 na gramu 1,140 za dawa za kulevya aina ya cocaine na kuhukumiwa kwenda jela miaka 20 na kutozwa faini ya Sh 148.1 milioni.

Kesi nyingine ni ya raia wa Nigeria Chukwudi Okechukwu na wenzake watatu, Paul Ikechukwa Obi, Shoaib Muhammad Ayaz na Hycenth Stan ambao walihukumiwa jela miaka 30 kila mmoja na kulipa faini ya Sh9 bilioni. Chukwudi na wenzake walibeba kilo 81 za dawa za kulevya aina ya heroine.

Mtuhumiwa mwingine aliyehukumiwa hivi karibuni alitambulika kwa jina moja la Fred, alikamatwa na kilo 180 za heroine maeneo ya Mbezi Jogoo na kuhukumiwa jela miaka 20 na kulipa faini ya Sh15 bilioni.

Kamanda Nzowa alisema kukamatwa kwa watuhumiwa wa dawa za kulevya hakuna ujuzi bali ni taarifa zinazoletwa na wasamaria wema ndizo zinazosaidia.

“Mashine ya X-ray peke yake haisaidii chochote, lakini taarifa zinazotusaidia ni zile zinazoletwa na raia wema halafu sisi tunazithibitisha kwa mashine maalum ya poligrahic,” alisema.

Alisema mashine hiyo inawasaidia kugundua mtu kasema uongo au ukweli pindi anapopeleka taarifa katika kitengo hicho.

Wasamaria wema wakituambia, sisi tunaanza kazi mara moja, tunahakikisha kama taarifa ni za kweli kwa kutumia mashine hiyo, inatueleza kama mtu anasema kweli,” alisema.

«
Next

Chapisho Jipya

»
Previous

Taarifa za zamani

About Unknown

Asante kwa kutembelea SELASINI HABARI,NITAKUHABARISHA, KUKUELIMISHA NA KUKUBURUDISHA HIVYO USIKOSE KUTEMBELEA SELASINIHABARI.BLOGSPOT.COM.

Hakuna maoni :

Leave a Reply